The Rock City Marathon 2012 Event 2012 Event The Rock City Marathon

Thursday 11 September 2014

Malinzi azindua Rock City Marathon 2014

Mratibu wa Rock City Marathon  kutoka kampuni ya Capital Plus International Ltd, Bi Grace Sanga (wa kwanza kulia) akipongezwa na Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT) Bw. Dioniz Malinzi (Wa nne kulia) ambaye alikuwa Mgeni Rasmi katika uzinduzi  wa Rock City Marathon 2014, jana jijini Dar es Salaam jana. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Baadhi ya wawakilishi wa wadhamini wa mbio za Rock City Marathon 2014 pamoja na viongozi wa chama cha mchezo wa riadha Tanzania, wakifuatilia yanayojiri wakati wa uzinduzi wa mbio hizo jana iliyofanyika Jijini Dar es Salaam. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Msemaji wa Kampuni ya Capital Plus International, ambao ni waandaaji wa mbio za Rock City Marathon, Bw. Mathew Kasonta, akizungumuza na wageni waalikwa katika uzinduzi wa mbio hizo jana iliyofanyika Jijini Dar es Salaam. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Afisa Uhusiano Mwandamizi wa Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF ) Bw. Jumanne Mbepo, ambao ndo wadhamini wakuu wa mbio za Rock City Marathon 2014, akizungumza machache wakati wa uzinduzi wa mbio hizo iliyofanyika Jijini Dar es Salaam jana. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Katibu Mkuu wa Shirikisho la Riadha Tanzania (RT), Suleiman Nyambui akizungumza machache wakati wa uzinduzi wa mbio hizo iliyofanyika Jijini Dar es Salaam jana. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Afisa Uhusiano na mawasiliano wa TSN Group Koiya Kibanga, ambao ni moja wa  wadhamini wakuu wa mbio za Rock City Marathon 2014, akizungumza machache wakati wa uzinduzi wa mbio hizo iliyofanyika Jijini Dar es Salaam jana. Mbio hizo zitafanyika tarehe 26 Oktoba katika uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Na Mwandishi Wetu,
Mwenyekiti wa Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Bw. Dioniz Malinzi, amezindua rasmi mbio za Rock City Marathon, zitakazofanyika Oktoba 26 mwaka huu kwenye Uwanja wa CCM Kirumba jijini Mwanza.
Akizungumza katika uzinduzi huo jana jijini Dar es Salaam, Malinzi alisema mbio hizo zimeweza kuwa ni moja ya mbio zinazoheshimika nchini Tanzania na kuiweka kanda ya ziwa katika kalenda ya michezo kila mwaka.
Malinzi aliipongeza kampuni ya Capital Plus International (CPI) kwa kuendelea kujidhatiti katika maandalizi ya mbio hizo na kuziboresha kila mwaka licha ya changamoto nyingi zinazoukabili mchezo huo wa riadha nchini.
 “Ni kweli kwamba makampuni na hata watu binafsi wamekuwa wakisaidia kukuza mchezo wa riadha hapa nchini, lakini bado mchezo huu unachangamoto nyingi.
“Jitihada za pamoja zinahitajika baina ya serikali kupitia Wizara ya Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo, sisi Baraza la Michezo la Taifa (BMT), vyama vya michezo, mashirika na wadau wengine, ili kurejesha heshima iliyopotea miongoni mwa michezo na wanamichezo wa Tanzania, hususani riadha,” alisema Bw. Malinzi.
Bw. Malinzi alibainisha kuwa na kuwepo kwa changamoto mbali mbali CPI imekuwa ikijitahidi kuboresha mbio hizo zifanyikazo kila mwaka.
“Tumeshuhudia viwango vya mbio hizi vikipanda kila mwaka, ambapo ni kielelezo cha maandalizi mazuri yanayofanywa kwa kuzingatia viwango na sheria zilizo wekwa,” aliongeza  Bw. Malinzi.
Hata hivyo, Mwenyekiti huyo wa BMT alisisitiza kuwa vyama vya michezo pia vinapaswa kujiimarisha katika kuwaandaa wachezaji kabla ya kuwapeleka kushiriki katika mashindano ya kimataifa ambapo wachezaji hao wanabeba jina la nchi ya Tanzania.
“Hatunabudi kuimarisha msingi wetu katika kila aina ya michezo hapa nchini, kama bado tunayo ndoto ya kuirudisha ramani ya Tanzania katika ulimwengu wa michezo kama ilivyokuwa zamani,” alisisitiza.
Tukio hilo limewavutia wadau wengi wa michezo nchini, ikiwa ni pamoja na makampuni makubwa kama Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), Kampuni ya TSN Group Ltd, Bodi ya Utalii Tanzania (TTB), African Barrick Gold, Nyanza Bottlers, Mfuko wa Pensions (PPF), Sahara Communication, ATCL, New Mwanza Hotel, na New Africa Hotel ambao wamejitokeza kudhamini mbio hizo.
Kwa upande wake Mwakilishi wa kampuni ya Capital Plus International, Bw. Mathew Kasonta, alisema mbio za mwaka huu zitahusisha mbio za nusu Marathon za kilomita 21, mbio za kujifurahisha maarufu kama Corporate Race za kilomita 5, mbio za watu wenye ulemavu wa ngozi za kilomita 3, mbio za watu wazima za kilomita 3 na mbio za watoto kuanzia miaka saba hadi 10 ambazo ni za kilomita 2.
Bw. Kasonta alisema kuwa mbio hizo zinaenda sambamba na kuhamasisha Utalii wa ndani kupitia sekta ya michezo, ambapo washiriki watakua ni kutoka kanda ya ziwa Victoria na nchi jirani kama Kenya, Uganda, Afrika Kusini na baadhi yao wakiwa na uzoefu wa kucheza mashindano ya kimataifa ili kutoa ushindani zaidi.
“Ningependa kutoa shukrani zangu za dhati kwa wafadhili mbalimbali wanaoshirikiana nasi ili kuyafanikisha mashindano haya, kwa niaba ya Capital Plus International, ningependa kuwahakikishia kuwa mashindano ya mwaka huu yataboreshwa zaidi na hivyo yataweza kutupatia wanariadha bora watakaoiwakilisha nchi yetu kikamirifu katika mashindano ya kimataifa,” alisema Bw. Kasonta.

Monday 8 September 2014

Rock City Marathon 2014 kuzinduliwa keshokutwa

Na Mwandishi Wetu

UZINDUZI wa msimu wa sita wa mbio za Rock City Marathon 2014 zilizoanza mwaka 2009, zikiwa na lengo la kukuza Utalii wa Ndani kupitia michezo, unatarajia kufanyika Septemba 10, kwenye Hoteli ya New Afrika, jijini Dar es Salaam.
Akizungumza jijini Dar es Salaam jana, Mratibu wa mbio hizo, Bi. Grace Sanga, alisema kuwa baadhi ya wanariadha, viongozi wa vyama vya riadha, viongozi wa Baraza la Michezo Tanzania na wadau mbali mbali wa mchezo wa riadha nchini wanatarajiwa kuhudhuria uzinduzi huo.
Bi. Grace alisema kuwa pamoja na maandalizi ya mbio za mwaka huu za Rock City Marathon kuboreshwa zaidi  ukilinganisha na miaka iliyotangulia, wawakilishi wa wanariadha na viongozi mbali mbali watapata fursa ya kuzungumzia changamoto zinazokumba mchezo wa riadha nchini na jinsi ya kukabiliana nazo.
“Tuko tayari kwa mbio za Rock City Marathon 2014, zitakazofanyika Oktoba 26. Kamati ya Maandalizi imeweka mikakati mizuri ili kuhakikisha mbio za mwaka huu zinakuwa bora na zenye mafanikio kulinganisha na misimu iliyopita,” alisema Bi. Grace.
Mratibu huyo alisema kuwa kwa kutokana na uendeshaji wa kuridhisha wa mbio hizo, wadhamini wengi wamejitokeza kuwezesha kuzifanya mbio hizo kuwa bora zaidi mwaka huu.
“Baada ya kufanya maandalizi ya Rock City Marathon kwa mafanikio kwa miaka tano mfululizo na kuweza kupandisha kiwango chake, makampuni na mashirika mengi yamejitokeza kudhamini mbio za mwaka huu kwa lengo la kuiboresha zaidi. Miongoni mwa wadhamini wetu mwaka huu ni pamoja na NSSF, TSN Group, African Barrik Gold, IPTL, TTB, TANAPA, New Mwanza Hotel, Nyanza Bottling Company, Sahara Communications, New African Hotel, Continental decoders, ATCL, PPF, Umoja Switch, and Bank M,” alisema Bi. Grace.   
Rock City Marathon zinaandaliwa na Kampuni ya Capital Plus International (CPI), kwa ushirikiano na Chama cha Riadha Tanzania (RT), pamoja na Chama cha Riadha mkoa wa Mwanza (MRAA), ambazo zimewavutia washiriki wengi wa ndani na nje ya nchi.
Bi. Grace aliongeza kwamba, mbio hizo zitakuwa na vipengele vitano kwa msimu huu, ambavyo ni mbio za kilometa 21 (wanawake na wanaume) na zile za kilometa tano kwa wakimbiaji kutoka makampuni mbalimbali, kilometa tatu kwa watu wenye ulemavu, kilometa tatu kwa watu wazima (zaidi ya miaka 55) na kilometa mbili kwa watoto walio kati ya miaka 7 mpaka 10.
“Tunatarajia watu wengi kujitokeza mwaka huu, kwa kuwa tumejipanga vizuri kwa msimu huu. Tumejifunza kupitia mbio za mwaka jana, hivyo Kamati ya Maandalizi imekuja na mpango madhubuti utakaoboresha mbio zetu kwa mwaka huu,” alisema Bi. Grace.

Monday 9 June 2014

Mbio za Rock City Marathon 2013 zafana

Na Mwandishi wetu
WANARIADHA Alphonce Felix kutoka Arusha na Vicoty Chepkemoi kutoka Kenya wameibuka vinara katika mashindano ya riadha ya kilometa 21 yanayojulikana kama ‘Rock City Marathon 2013’ yaliyofanyika Jijini Mwanza jana Jumapili nakujinyakulia Shilingi milioni moja na nusu (Sh 1.5 m) kila mmoja.
Alphonce alishinda mbio hizo kwa upande wa wanaume baada ya kutumia saa 1:02:17 hivyo kuvunja rekodi iliyowekwa mwaka jana na mwanariadha Kopiro Chacha aliyetumia 1:05:00, huku Chepkemoi aki kutumia 1:12:44.
Nafasi ya pili alishika Joel Kimtiae wa Kenya kwa upande wa wanaume na Sarah Ramdhani kutoka Arusha kwa upande wa wanawake, wakifuatiwa na Sambo Andrea kwa upande wa wanaume na Zakia Mrisho kwa upande wa wanawake wote wakitokea Tanzania.
Zaidi ya wanariadha 1090 walijitokeza kushiriki mashindano hayo yanayoandaliwa na kampuni ya Capital Plus International kwa mwaka wa tano mfululizo.
Wambura Lameck kutoka Holili alingara katika mbio za kilometa tano huku Dotto Ikangaa kutoka Arusha akishika nafasi ya pili .

Kwa mujibu wa waratibu wa mbio hizi, udhamini waliopata kutoka kwa wadamini ambao ni, Mfuko wa Hifadhi ya Taifa ya Jamii (NSSF), Africa Barrick Gold (ABG), Precision Air, Airtel kupitia Airtel Money, TANAPA, Bank M, PPF, Nyanza Bottling Ltd, New Mwanza Hotel, Sahara Communications, Continental Decoders na Umoja Switch, umewawezesha kuboresha tuzo kwa washiriki pamoja na kufanya maadalizi mazuri yanayozingatia sheria za riadha.
Washiriki na washabiki wa mbio za Rock City za mwaka huu walipata kuburudishwa na kikundi cha Sanaa cha Bujora ambacho kilionyesha umahiri wake wa kuonyesha utamaduni wa kitanzania kupitia dansi.         
Mwakilishi wa Mkuu wa mkoa wa Mwanza Bw Kizito Bahati (Afisa michezo Manispaa ya Ilemela), mbali na kutaka washiriki kutoka kanda ya ziwa kuchangamkia fursa inayoletwa na mbio hizo, pia aliwataka viongozi wa vyama vya riadha kuwa na program endelevu ya kukuza mchezo wa riadha kwa kushirikiana na Maafisa Michezo wa Mikoa na Wilaya ili waweze kupata fursa ya kufikisha na kuufundisha mchezo huu katika shule ambako ndio chimbuko la vipaji vya michezo.
“Nawashukuru sana waandaaji wa mbio hizi za Rock City Marathon kwa kuweza kuandaa shindano ambalo limeweza kutusaidia sisi wadau wa riadha kugundua vipaji vingi ambavyo tunavyo hapa nchini. Hivi vipaji vinastahili kukuzwa. Hivyo basi natoa wito kwa watu wote wenye dhamana ya michezo kutumia mbio hizi kama chambo cha kuweza kutambua vipaji vingi vya riadha ambavyo vinahitaji kuendelezwa kwa manufaa ya taifa,” alisema Bw Kizito.
Pamoja na hayo mashindano haya yameweza kufanikiwa kwa udhamini wa makampuni mbalimbali nayapongeza kwa juhudi zao za kuweza kuinua michezo hapa mkoani Mwanza na Tanzania kwa ujumla. Nayaomba na makampuni mengine kujitokeza kudhamini michezo hii kwani fursa kwao katika kutangaza bidhaa zao.

Mshindi  wa kwanza wa mbio za Rock City Marathon 2013 kilomita 21 kwa upande wa wanaume Alphonse Felix kutoka mkoani Arusha akimalizia mbio hizo kwenye uwanja wa CCM Kirumba ambapo alitumia saa 1:02:17 na kufanikiwa kuvunja rekodi iliyowekwa mwaka jana na Opio Chacha aliyetumia saa 1:05:47.

Powered by Blogger.